Kalameni aliyechanganyikiwa kwa kutafuna miraa, aliwashangaza  jirani zake alipotembea kilomita sita akitafuta kiberiti ili awashe sigara yake.

Kalemeni huyo alianza kutafuna miraa kibarazani mwendo wa saa tano asubuhi huku akiburudika na kidundo taratibu ya taarab.

Ilipofika saa tatu unusu za usiku, baadhi ya majirani zake waliamua kuondoka hali yeye akiendelea kutafuna miraa. Lakini ilipofika usiku wa manane, Kalameni alionekana mwenye wasiwasi huku akitiririkwa na jasho mithili ya mchezaji hodari wa mieleka aliyeshuka kutoka ulingoni.

“Aise , sina kiberiti itakuwaje na ndiyo handas imepanda na nataka kuvuta sigara? Kalameni akasikika akijiuliza pasipo kupata  jibu.
Alitapatapa huku na kule akitazama kama angepata angalau mshale wa kiberiti lakini hakufaulu.

Kwa vile ilikuwa ni usiku wa manane, Kalameni aliogopa kwani badhi yao walisikika waking'orota kwa usingizi wa mang'amung'amu.

Aliwaza na kuwazua jinsi angepata kiberiti ili azime kiu yake lakini hakuwa na njia.  Ndipo akaamua kwamba lisilo na budi hutendwa!

Alianza kweda Katoloni madukani akiwa na matumaini makubwa kwamba angepata baadhi ya maduka yakiwa wazi.  Lakini masikini maduka yote yalikuwa yamefungwa na ndipo akaamua kushika kiguu na njia hadi mtaa jirani wa  Kirang'o lakini huko pia maduka yalikuwa yamefungwa.
Hata hivyo alipofika hatua chache tu kufika Kabondo mjini, handas zikaanza** kukatika na baadaye kajiuliza sababu zilizomfanya kufika umbali huo, akakosa jibu muafaka.

“Duuuh! Umbali huu wote eti natafuta kiberiti ili nivute sigara?  Ajabu!” Kalameni  akashangaa na kutafuta namna ya kurudi kwake.